• Michezo Kimataifa 1/5

    Kiungo wa kati wa Liverpool Phillipe Coutinho ni moto wa kuotea mbali katika lango la Arsenal Mshambuliaji wa Arsenal Olivier Giroud atakosa mechi ya Ijumaa pamoja na mechi kadhaa za wakati wa likizo kutokana na jeraha la nyuma ya goti.

  • Bill Clinton na mkewe Hillary Clinton 2/5

    Mshauri mmoja wa mgombea wa urais nchini Marekani Donald Trump ,amesema kuwa mfanyibiashara huyo bilionea huenda akatumia mjadala wa Jumatatu kuzua historia ya uhusiano wa kimapenzi wa Bill Clinton.

  • Waziri wa Ulinzi amewatembelea wanajeshi wa Tanzania nchini DRC 3/4

    Ikiwa zimepita siku 16 tangu kuuawa kwa askari 14 wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) waliokuwa kwenye oparesheni ya ulinzi wa amani katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Waziri wa Ulinzi wa Tanzania Husssein Mwinyi amewatembelea wanajeshi wa Tanzania waliopo nchini humo.

  • Hifadhi ya taifa ya mlima Kilimanjaro 4/4

    Kilimanjaro ni miongoni wa vilele virefu vinavyofikika duniani, ni alama kwa wageni wengi kutoka duniani kote yenye kilomita za mraba 1668 (maili za mraba 641), kaskazini mwa Tanzania, karibu na mji wa Moshi wapandaji mlima wengi wanafika katika ukingo wa Kreta kwa kutumia fimbo ya kutembelea, mavazi yanayofaa na nia thabiti.

Jeshi la Uganda ladai kuwaua waasi wa ADF DR Congo

Waasi wa ADF wanaopetekeleza opresheni zao mashariki mwa DR Congo
Jeshi la Uganda linasemekana kushambulia kambi kadhaa za waasi mashariki mwa Congo.
Kwa mjibu wa msemaji wa jeshi la UPDF, shambulio hilo lilifaulu baada ya Uganda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, kugawana taarifa za kijasusi.
Kwa upande wake, msemaji wa serikali ya DR Congo Richard Karemire, ameviambia vyombo vya habari nchini humo kuwa, ni ukweli kwamba wanajeshi wa Uganda wamevamia maeneo ya waasi na kushambulia kambi kadhaa.
Ameongeza kusema kuwa, wanajeshi hao wa Uganda hawakuingia nchini DRC, bali walitumia ndege za kijeshi pamoja na makombora mazito mazito ya kulipua mbali.
Idadi ya waasi waliouwawa bado haijatolewa.
Waasi hao wa ADF hivi majuzi walidaiwa kupanga mashambulio dhidi ya wanajeshi walinda amani wa MONUSCO.
Share:

Korea Kaskazini: Marekani inapanga kutekeleza ''uhalifu''

Marekani imemuonya rais Kim Jong Un wa Korea Kaskazini kusitisha majaribio yake ya silaha
Katika siku ambayo baraza la usalama la Umoja wa mataifa linapiga kura kuidhinisha vikwazo vikali zaidi dhidi ya Korea kaskazini, kiongozi wa taifa hilo, Kim Jong-un, amesema taifa lake linawakilisha tishio kubwa la nyuklia kwa Marekani.
Katika hotuba iliyoripotiwa na shirika la utangazaji habari nchini (KCNA) Kim amesema kuendelezwa kwa haraka kwa mpango wa nchi yake wa nyuklia kunashinikiza ushawishi muhimu katika siasa za kimataifa.
Azimio la hivi karibuni la baraza hilo la usalama katika Umoja wa mataifa linalenga kupiga marufuku usafirishaji wa bidhaa zote za mafuta kwenda Pyongyang na kuitisha kurudishwa kwa raia wa Korea Kaskazini wanaofanya kazi katika nchi za nje katika muda wa mwaka.
Korea Kaskazini imetaja nakala za kiusalama za Marekani zinazosisitiza kuhusu utumizi wa mabavu dhidi ya Pyongnyang kuwa za kihalifu, vyombo vya habari vya taifa hilo zimesema.
Wizara ya maswala ya kigeni ilimlaumu rais wa Marekani Donald Trump kwa kutaka kukandamiza ulimwengu kupitia sera yake mpya ya usalama.

Rais Trump amesema kuwa Marekani itatumia nguvu dhidi ya Pyongyang
Rais Trump amesema kuwa Marekani itatumia nguvu dhidi ya Pyongyang
Siku ya Jumatatu rais Trump alisema kuwa Washington lazima ikabiliane na changamoto inayoletwa na mpango wa kutengeza silaha wa Pyongyang.
Msemaji wa wizara ya maswala ya kigeni nchini Korea Kaskazini amesema kuwa mpango mpya wa Marekani kuhusu usalama hauna lolote bali mpango wa kutaka kutumia nguvu kulingana na chombo cha habari cha kitaifa KCNA.
Ameilaumu Marekani kwa kutaka kujaribu kuvuruga taifa hilo na kugeuza rasi yote ya Korea kuwa eneo litakalotawaliwa na Marekani.
Siku ya Jumatatu rais Trump alielezea kuhusu mpango huo mpya akiikosoa Korea Kaskazini kwa kufanya majaribio ya silaha za kinyuklia licha ya shutuma kutoka Marekani na Umoja wa Mataifa.
Mwezi uliopita, rais wa Marekani pia aliliweka taifa la Korea Kaskazini miongoni mwa mataifa yanayofadhili ugaidi.
Share:

Hukumu ya Lulu: Yapo mengi ya kujifunza


HUKUMU ya Elizabeth Michael ‘Lulu’ kwenda Jela miaka miwili sawa na kumaliza msiba wa marehemu Steven Kanumba, hii ina maana amezikwa tena kifikra, kwa mujibu wa mama yake mzazi Flora Mtegoa.
Haki imetendeka hukumu imetolewa ni muda mwingine wa kuangalia yale ambayo yalitokea ili iwe funzo kwetu tuliobaki uraiani na bado tumepewa nafasi ya kuishi. Mapema wiki hii, Mahakama Kuu kanda ya Dar es Salaam ilimhukumu jela miaka miwili Lulu baada ya kumkuta na hatia kwa kumuua Kanumba, Aprili 2012.
Hili liwe funzo kwa Wanatasnia zote mbili kwa muziki wa Bongofleva na Filamu, liwe funzo kwa Wazazi pia liwe funzo kwa Serikali na kila binaadamu kwakuwa siku na saa yoyote huenda likamtokea mwingine sababu hata wao hawakutarajia.
Wasanii liwe funzo kubwa kwao, ukizingatia Lulu na Kanumba wote walikuwa wasanii wa tasnia ya filamu. Wasanii wajifunze sanaa sio chombo cha kuendeshwa kwa rushwa ya ngono, kwaajili ya kumsaidia mtu afikie malengo yake, wawe na msimamo wamsaidie mtu kama wanaweza kama hawawezi wamwache aende kutafuta rizki kwingine.
Lakini sio kutumia sanaa kumlaghai mtu kwa kumwaminisha kwamba utamtoa katika sanaa yake, kumbe ulikuwa na lengo la kumtumia kwa kuchukulia kigezo cha shida zake na umri wake.
Najua wasanii wengi watakataa kwamba hawana mahusiano na wasanii wachanga, ambao wanatamani kuigiza huku umri wao ukichini ya miaka 18 tena wengine wakiwa shuleni.
Najua watakataa kwamba wao wanamashabiki wengi wanawake, lakini kundi kubwa la mashabiki hao ni wanafunzi wa Sekondari na shule za msingi ambao wengi wanandoto za kuwa na umaarufu mkubwa kama wa Wema Sepetu, Jackline Wolper au Kajala Masanja.
Wajifunze kwa mfumo wa kesi ya Lulu ulivyokuwa ukienda, ingekuwaje kama Kanumba asingekufa? Leo ingekuwa aibu ya mwaka kwa kutembea na mtoto wa miaka 16. Na pengine katika kukwepa hilo ndio maana uhusiano wa waili hao ulikuwa wa siri, hakuna aliyefahamu mpaka baada ya tukio la kifo cha Kanumba, ndipo siri ilipofichuka kwamba wawili hao walikuwa wapenzi.
Watu wa haki zote tungewasikia, huenda hukumu ya Lulu ingekuwa yake, kwa kesi ya kubaka ambapo tunajua kabisa ni miaka mingapi angetumikia jela. Hivyo hukumu ya Lulu na kifo cha Kanumba iwe somo kwa wasanii wengine, kwakuwa makosa kama hilo linaweza kutokea kwa mwingine kwakuwa maisha hayana mfumo maalumu wa kuelekea.
Unaweza usipatwe na umauti kama ilivyokuwa kwa Kanumba, lakini ukadhalilika kwa kuingia jela miaka 30 kwa kujihusisha kwenye uhusiano wa kimapenzi na mtoto aliye chini ya umri wa miaka 18.
Hata hivyo hatutaacha kumkumbuka Kanumba, kwakuwa msaada wake wa kuinua tasnia ya filamu ni mkubwa, ingawa kifo chake kimezua maswali mengi na mafunzo yasiyokuwa na mwisho.
Lakini pia kilichomkuta Lulu, iwe funzo kwa wazazi na walezi wenye watoto aina yake, wawe wapo kwenye filamu, muziki au wanafunzi. Mtoto anabaki kuwa mtoto na mzazi ama mlezi wake lazima azingatie misingi ya kumlea mtoto, ukuaji wa Lulu sababu ya umaarufu wake haikuwa siri ya alichokuwa akikifanya, kwani mara kwa mara alikuwa akipamba kurasa za magazeti ya udaku, mara kalewa chakari harusini, mara kakutwa kwenye kumbi za burudani.
Mtoto wa chini ya umri wa miaka 18 anafuata nini kwenye kumbi za starehe? Mtoto mwenye umri wa chini ya miaka 18 anaendaje harusini peke yake na kulewa?. Lawama hizi pia ziende kwa wasanii wenzake wakubwa wakati huo ambao walikuwa wakienda nae kwenye harusi na kumuacha analewa, huku wakifahamu fika kwamba licha ya kuigiza nae, lakini huyo ni mtoto bado.
Miaka Fulani uongozi wa ukumbi wa Bilicanas uliwahi kumtoa nje Lulu, kwa madai ya kuingia klabu za usiku akiwa na umri chini ya miaka 18. Na siku chache baadae alifanya sherehe kuadhimisha siku ya kuzaliwa akidai ametimiza umri wa miaka 18, lakini kabla ya hapo aliwahi kutamba kumiliki hati ya kusafiria ya mtu mzima na ana uwezo wa kusafiri popote, lakini hakuna yeyote aliyezungumza juu ya hilo si wazazi wake waka wasanii wenzie waliomzidi umri ambao wakati huo wengi walikuwa na umri sawa na mama zake, dada zake, baba zake ama kaka zake.
Suala la kutokuwa na umri wa miaka 18, lilikuja kufichuka baada ya kifo cha Kanumba, ndipo ilipobainika kuwa alidanganya umri ili iwe rahisi kwake kufanya mambo ya kikubwa kama kwenda kwenye kumbi za burudani na mambo mengine.
“Nilikuwa kila nikienda klabu nazuiwa mlangoni, naambiwa mimi mdogo… nikafikiria nikaona ngoja nifanya ‘birthday’ kisha nitangaze nimefikisha miaka 18, lakini lengo lilikuwa nisiwekewe tena vizuizi kwenda klabu,” alisema Lulu kwenye moja ya mahojiano yake na vyombo vya habari miaka ya nyuma.
Wazazi wake walikuwa wapi wakati mtoto wao anatanagaza hadharani kuwa na miaka 18 tena kwa lengo ovu, kwanini wasingemzuia? Mzazi anayemlea mtoto wake kwa maadili ni lazima angejiuliza sababu za mtoto tena binti kufanya hivyo.
Kwa mujibu wa ushahidi wake Mahakamani, siku ya kifo cha Kanumba, Lulu alikuwa anaenda ‘kujirusha’ na rafiki zake, mama yake alimruhusu vipi? Mtoto wa chini ya miaka 18 anatokaje usiku na marafiki na mzazi roho iwe tuli.
Wazazi wengi katika sanaa ya filamu na muziki, wamekuwa hawaulizi mali ambazo watoto wamekuwa wakizipata, hata kudadisi ingawa magazeti yanakuwa yanaandika ukweli. Wazazi wamekuwa kimya kwa kuamini kwamba wanakula matunda ya watoto wao, hivyo linapotokea tatizo ndipo wanaposema mwanetu alikuwa akibakwa.
Ni bora kuziba ufa hata kwa matope na miti, ili ukianguka uanguke wakati umeshahamia nyumba nyingine kuliko kuuacha kwa kusema kwa maneno ukuta usianguke mpaka nihame. Lakini pia kuna la kujifunza kwa Serikali yetu kupitia wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na michezo, kupitia kitengo chake cha Baraza la Sanaa Tanzania.
Magazeti yamekuwa yakiandika habari nyingi za wasanii kuhusiana na matendo yao ya kutoka usiku, kudanganya miaka na matukio ambayo yapo chini ya umri wao. Kwa mfano kupitia mitandao ya kijamii, baba mzazi wa mwanamitindo wa video maarufu kama Tunda, amekuwa akilalamikia baadhi ya msanii kumharibu mtoto wake.
Mzee yule aliongea mengi na magazeti mengi yaliandika kwamba mwanaye bado mwananfunzi, ila wanamuziki wanamtumia katika video zao na kumharibia maisha yake ya baadaye.
Niliwahi kumsikia mwigizaji mwingine Hanifa Daud Maarufu kama Jenifa wa Kanumba, naye miongoni mwa watu waliowahi kulalamika kwamba kuna unyanyasaji wa kijinsia katika tasnia ya filamu.
Lakini sijasikia kitengo chochote cha Serikali kinachohusiana na sanaa ambacho kikaivalia njuga habari hiyo, hata kwa kuhoji umri wa binti huyo. Labda kuweka wazi kwa baadhi ya vitu kama hivi kusaidia kesi kama hii ikitokea watu kupata majibu ya haraka, mepesi na kila mtu akapata haki stahiki kwa mujibu wa sheria.
Lakini wakisema wakae kimya basi kila msanii atakuwa akimchukua mtoto akimfundisha sanaa, akiwa mkubwa anakula matunda yake mwenyewe kwa kumfanya mpenzi wake, hapo ndipo watu watakapoacha kuwapeleka watoto wao kufanya sanaa.
Kisha tutaendelea kulalamika kwamba sanaa ya Tanzania haikuwi, ndio kwanza inakufa, mara filamu za nje zinaua filamu kumbe sisi wenyewe tunaendesha filamu ili kufanya mambo yetu.
Sina lengo la kushambulia upande wowote katika makala haya, bali nataka wadau wa sanaa, wazazi na watoto kujifunza kupitia hukumu ya Lulu. Leo Lulu amehukumiwa akiwa mtu mzima, akitoka gerezani atakuwa na maisha yake na baadae atakuwa na familia, lazima ahakikishe njia alizopita yeye watoto wake hawapiti, ajifunze malezi mazuri ya watoto wake kupitia makosa waliyofanya wazazi wake kwake mpaka leo kumkuta yaliyomkuta. Lala kwa amani Kanumba.
Share:

Sikujua tumbaku ingegeuka janga kwangu


ALIPOANZA kusokota tumbaku na kuvuta akiwa na umri wa miaka 24, Maine Mshomi aliichukulia kuwa ni kiburudisho. Hakuota abadani kwamba ‘kiburudisho’ hicho kingegeuka janga katika maisha yake.
Akiwa sasa na umri wa miaka 55, Mshomi ambaye ni mkazi wa kijiji cha Lugine wilayani Kiteto katika Mkoa wa Manyara, anakumbuka alivyokuwa akivuta misokoto ya tumbaku kati ya minne na mitano kwa siku. Tumbaku aliyokuwa akivuta alikuwa akiipata kijijini ambako inalimwa lakini si kwa ajili ya biashara bali kwa matumizi yao.
Anasema alipokuwa akienda katika maeneo yenye mkusanyiko wa watu, alikuwa akivuta sigara. Wakati mwingine alipatwa na mawazo ya kuacha kutumia tumbaku hususani alipokuwa hana fedha, lakini alipopata fedha aliendelea kuvuta.
Mshomi mwenye watoto wanne, anasimulia haya yote akiwa kitandani katika Hospitali ya Saratani ya Ocean Road, jijini Dar es Salaam. Amepimwa na kubainika kwamba anasumbuliwa na saratani ya koo.
Kabla ya kufika hospitalini hapo, alishakwenda hospitali nyingine kutafuta tiba bila mafanikio. Hospitali hizo ni Mvumi iliyopo mkoani Dodoma pamoja na KCMC ya mkoani Kilimanjaro.
Anasema amekuwa akijigharimia matibabu na sasa ameshatumia si chini ya Sh milioni 1.7. Samueli Mshomi ni ndugu yake wa karibu anayesimulia kuwa kaka yake alianza kuugua Machi mwaka huu na Ocean Road walifika Agosti mwaka huu.
“Kaka yangu amevuta tumbaku kwa muda mrefu sana, takribani kipindi cha chote ujana wake,” anasema Samueli. Anaongeza: “Tulimshauri kuacha alipoanza kuumwa japokuwa yeye mwenyewe hakuwa tayari kwa madai kwamba daktari hajamwambia kama ugonjwa wake umechangiwa na matumizi ya tumbaku.”
Hata hivyo, anasema maelezo ya daktari yalionesha moja kwa moja kuwa matumizi ya tumbaku yamechangia kwa kiasi kikubwa katika ugonjwa wa ndugu yao. Samuel anasema mpaka sasa kaka yake haamini kama tatizo lake limesababishwa na matumizi ya tumbaku akihoji kwamba mbona kuna wagonjwa wengine wanaugua saratani na hawajawahi kutumia tumbaku?
Samueli anasema ipo haja ya serikali kutoa elimu ya kutosha hasa kwa wakazi wa vijijini kuhusu madhara makubwa yanayoletwa na utumiaji wa tumbaku. Mkazi huyo wa kijiji cha Songambele anasema matumizi ya tumbaku yako juu sana kijijini kwao.
Anatamani ingewezekana, serikali izuie uzalishaji wa tumbaku kutokana na madhara yake kiafya. Wakati wa maadhimisho ya siku ya kupinga matumizi ya tumbaku Mei mwaka jana, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu alisema tafiti zinaonesha takribani watu milioni sita hupoteza maisha duniani kwmwaka kutokana na utumiaji wa tumbaku na bidhaa zake.
Akielezea uhusiano wa tumbaku na saratani, Mkurugenzi wa Huduma za Kinga ya Saratani katika Hospitali ya Taifa ya Ocean Road, Dk Chrispin Kahesa anasema tumbaku ina kemikali zaidi ya 200 na kati ya hizo 69 zinahusishwa na saratani.
“Saratani kwa ujumla ni mkusanyiko wa magonjwa zaidi ya 200, inategemea tu ni saratani ya eneo gani, mfano, titi, koo, shingo ya uzazi na kadhalika,” anasema. Anasema takribani saratani zote zinahusishwa na tumbaku lakini zaidi ni saratani zinazoathiri maeneo ya mfumo wa chakula.
Akifafanua kitaalamu, anasema mfumo wa chakula unaanzia kwenye kinywa ukihusisha ulimi, mdomo, njia za hewa koo na tumbo. “Kuna saratani nyingine zaidi zinaongezeka kama vile saratani za kibofu, mapafu, shingo ya kizazi na kadhalika kwa sababu hizi kemikali ukizivuta zinaingia kwenye nji ya hewa lakini zinasambaa kwenye damu hadi zinakwenda kuathiri maeneo mengine,” anasema.
Anaongeza: “Kwa hiyo tafiti zinaonesha zile saratani ambazo zinaanzia kwenye njia ya chakula na mfumo wa hewa unaohusisha pia mapafu ndizo huwaathiri wengi zaidi. Anasema athari za tumbaku siyo kwa wanaotumia kwa kuvuta pekee bali hata wanaomung’unya kama wala ugoro huathirika eneo la kinywa au njia ya chakula. Dk Kahesa anasema saratani za njia ya kinywa na chakula zinaongezeka nchini.
Anasema kwa wanaume saratani inayoongoza ni ya ngozi ikifuatiwa na ya njia ya chakula ambayo kwa kiwango kikubwa inachangiwa na matumizi ya tumbaku. Hata hivyo, anasema idadi ya wagonjwa inayoonekana hospitalini ni ndogo kwa maana upo uwezekano wa wengine kufariki bila kutambulika kutokana na kutopata fursa ya kufika katika maeneo ya tiba.
“Kwa mfano, ukienda Katavi kuna matatizo mengine ya kiafya ambayo yanaendana kabisa na matumizi ya tumbaku kama vile upungufu wa nguvu za kiume,” anasema. Anasema wengine wanaotumia tumbaku pia ni watumiaji wazuri wa vitu vingine hatarishi ikiwemo pombe.
“Tumbaku inaweza kuhamasisha matumizi ya vitu vingine lakini yenyewe kama yenyewe ni shida kuijua takwimu zake. Tunaweza kusema ni ya nne kwa sababu tumbaku imeguswa kwenye kila aina ya saratani kwa sababu ya kemikali zake kuchangia.
“Unaweza kusema asilimia 60 ya saratani inachangiwa na virusi lakini ukija kwenye tumbaku kila saratani imehusishwa na tumbaku,” anafafanua Dk Kahesa. Wakati baadhi ya watu (akiwemo Mshomi) wakijipa moyo kwa kusema ‘mbona watu wengine wanavuta sigara na hawaugui saratani, Dk Kahesa anafafanua kuwa maradhi hayo huchukua muda mrefu hadi kugundulika.
Anasema umri wa sasa wa kuishi kwa Tanzania ni miaka 62 na kipindi kilichopita ilikuwa miaka 52. Hivyo anasema wagonjwa wengi kipindi kilichopita walikuwa ni wazee wenye umri wa takribani miaka 65.
“Kwa hiyo utaona watu wengi walikuwa wanafariki kabla saratani haijatokeza. Kama wangeishi miaka 80 hadi 90 wengi wangegundulika, lakini walikuwa wanatibiwa kwa maradhi mengine kama vile TB (Kifua Kikuu).
Wengine wanasema hawaoni ugonjwa wowote lakini ukweli ni kwamba vifaa vya kugundua saratani ni vya utaalamu wa hali ya juu.” Mbali na saratani, uvutaji tumbaku/ sigara pia unachangia maradhi ya moyo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Dk Mohamed Janabi anasema athari kubwa za matumizi ya tumbaku zinakuwa kwenye mishipa ya damu ya moyo. Anafafanua kwamba moyo umezungukwa na mishipa ya damu inayoitwa coronary arteries ambayo sigara huwa inaiharibu.
“Kwa Tanzania bado uvutaji wa sigara siyo tatizo kubwa, bado halijawa kubwa, hatuwezi kuweka sigara katika orodha ya juu. Lakini wagonjwa wetu waulizwe kuhusu sigara kwa sababu ni moja ya magonjwa ya moyo. Asilimia 60 ya mgonjwa anaumwa nini tunaipata katika historia ya mgonjwa.
“Kuna wagonjwa wa moyo hapa ambao unasikia wanavuta pakiti mbili hadi tatu kwa siku, athari yake inakuwa kubwa zaidi, kwanza nafasi yake ya kuharibu mishipa ya moyo inakuwa kubwa sana na uachaji wake unakuwa mgumu kwa sababu mtumiaji atapata kitu kinaitwa withdrawer syndrome ambazo ni nyingi kidogo,” anasema.
Hata hivyo, anasema wagonjwa wanaowahudumia hospitalini hapo kwa sababu ya uvutaji wa sigara ni wachache kulinganisha na wale ambao wanapata tatizo la mishipa ya damu kutokana na mafuta na uzito.
Hata hivyo, Dk Janabi anasema ni muhimu Tanzania kuingilia kati matatizo yatokanayo na tumbaku kabla tatizo halijawa kubwa sana. Anatoa mfano akisema zipo nchi zilizoweka udhibiti wa uvutaji wa sigara.
Mfano Australia, mtu hawezi kuvuta kwenye eneo la chuo, Uingereza huwezi kuvuta kwenye baa na wala kubandika matangazo ya sigara kama vile kwenye mashindano ya magari.
Dk Janabi anasema ndani ya sigara kuna kemikali ya nikotini ambayo ina uraibu (hali ya mwili kuzoea kitu fulani). “Ikikuzoea uachaji wake unakuwa mgumu na ndiyo maana ni muhimu vyombo vya habari vikaendelea kuelimisha watu kuepuka kuvuta sigara kwa sababu ukishaanza kuvuta uwezakano wa kuacha unakuwa mgumu,” anasema Dk Janabi.
Anasema elimu inapaswa itolewe kwa wananchi kuhusu athari za sigara na ndiyo maana kwenye paketi za sigara zimeandikwa ‘uvutaji wa sigara ni hatari kwa afya yako’. Kwa kuzingatia athari zake, Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) lilitunga Mkataba wa Kimataifa wa Kudhibiti Tumbaku (WHO FCTC).
Nchi 180, zimeridhia mkataba huo ikiwemo Tanzania iliyouridhia Aprili 2007. Chama cha Kudhibiti Tumbaku Tanzania kupitia kwa mwenyekiti wake, Lutgard Kagaruki kinasisitiza kuwa tumbaku ni janga la taifa ambalo serikali katika kupambana, inapaswa isaidie wakulima kujikita kwenye mazao mbadala na kuwapatia masoko bora na ya uhakika.
“Kwa kuepuka tumbaku, taifa litakuwa limeokoa kizazi cha sasa na kijacho dhidi ya majanga ya kiafya, kiuchumi, kijamii na kimazingira, yanayosababishwa na kilimo na matumizi ya tumbaku,” anasema Kagaruki.
Share:

Takukuru, Waziri Dk Philip Mpango waikaba koo Airtel


SIKU moja baada ya Rais John Magufuli kuagiza Kampuni ya Simu ya Airtel kurejeshwa serikalini, Waziri wa Mipango na Uchumi, Dk Philip Mpango ameitisha vikao vya mfululizo kutwa nzima jana ili kuanza kuchunguza suala hilo, kwa lengo la kupata majibu.
Katika hatua nyingine, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) nayo imesema imeanza kufanya uchunguzi wa kina juu ya suala hilo ili kukamilisha agizo la Rais Magufuli juu ya upatikanaji wa majibu ya sakata la Airtel kwa wakati. Juzi Rais Magufuli alimuagiza Waziri Mpango kuifuatilia Airtel ili kujua ukweli ili umiliki wake urudi serikalini kabla ya kuisha kwa mwaka huu.
Gazeti hili jana lilifanya juhudi za kumpata Waziri Mpango ili kujua mkakati wake wa kulishughulikia suala hilo kutokana na muda mfupi aliopewa na Rais Magufuli na kubaini kuwa kwa siku nzima jana, alikuwa akiendesha vikao vilivyokuwa vinajadili suala hilo. Kupitia simu yake ya mkononi, mtu mmoja aliyejitambulisha kuwa ni msaidizi wake aliliambia gazeti hili kuwa Waziri Mpango, alikuwa akihudhuria vikao vinavyojadili suala la Airtel.
“Sijui una shida gani, lakini tangu asubuhi Waziri yupo katika vikao, ni vigumu kwake kuzungumza na wewe wakati huu na nafikiri hata baadaye hataweza, maana vikao hivi haviwezi kuisha mapema. “Kama unavyojua jana kuna maelekezo yaliyotolewa na Rais (Magufuli) kwake, hivyo tangu asubuhi yupo katika vikao vinavyohusu suala hilo, hivyo sina hakika kama unaweza ukapata nafasi ya kuzungumza naye kwa leo,” alisema msaidizi wake huyo.
Takukuru yaanza uchunguzi Katika hatua nyingine, gazeti hili lilimtafuta msemaji wa Takukuru, Musa Misalaba ili kujua ni kwa namna gani taasisi hiyo imeanza kulifanyia kazi suala hilo kutokana na kuonekana wazi kuwepo mazingira ya rushwa, ambapo alisema tayari wameanza kufanya uchunguzi. “Kuhusu suala la Airtel, hata sisi tumesikia agizo la Rais, lakini kama mnavyojua ni suala linalohusu uchunguzi kwa hiyo tumeanza kulishughulikia.
Wakati wowote baadaye tukiwa tayari tutawapa taarifa,” alisema. Bodi ya TTCL yajitosa Aidha, katika hatua nyingine, Bodi ya Wakurugenzi ya Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL), imeiomba serikali kusaidia kurejeshewa kampuni ya Airtel, kwa kuwa umiliki wake si sahihi na umejaa udanganyifu mwingi.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa Bodi ya TTCL, Dk Omar Nundu, alisema hakuna ubishi kuwa Airtel ni mali ya serikali chini ya TTCL, hivyo ni muhimu wakarejeshewa wakati huu, ambao kampuni hiyo imeingia katika mapambano ya kiuchumi.
Alisema itakuwa ni usaliti, iwapo Bodi ya TTCL na uongozi wa kampuni hiyo, hawatautoa hadharani ukweli kuhusu uhalali wa Airtel, na kwamba wamejitoa sadaka kuinyanyua TTCL iweze kupeleka gawio la kutosha serikalini.
Dk Nundu aliyewahi kuwa Waziri wa Uchukuzi katika Serikali ya Awamu ya Nne, alisema dhuluma iliyofanywa kwa kipindi chote cha utendaji wa Airtel itawekwa wazi mbele ya Watanzania na kwamba alichokifanya Rais Magufuli ni kuchokoza na wao wako tayari kutoa ushirikiano ili kampuni hiyo iweze kurudi.
Kwa mujibu wa Nundu, kikao kilichowakutanisha viongozi mbalimbali wakiwemo wa Kampuni ya Celtel na serikali kilichofanyika Agosti 5, mwaka 2005, kilijawa na maamuzi yenye vioja yaliyoifikisha Airtel mahali ilipo sasa.
Alisema kurudishwa kwa Airtel ni vita kubwa, wanayokwenda kupambana nayo kwa sasa huku wakiamini kuwa wapo watakaopata msukosuko, lakini wanachokiamini ni kurejea kwa kampuni hiyo ya Airtel chini ya utendaji wa TTCL.
“Hasara nyingi tumeipata tangu kuanzishwa kwa kampuni hiyo, tumewekeza mitaji mingi, ndio maana tunasisitiza kuwa upo ushahidi kuwa ni mali ya TTCL kwa asilimia 100,” alisema Nundu. Kwa upande wake, Ofisa Mtendaji Mkuu wa TTCL, Waziri Kindamba alisema uongozi wa TTCL na wafanyakazi wote, wanaiunga mkono Bodi ya TTCL kwa asilimia 100 kutokana na mkakati wake wa kusimama kidete ili kuirejesha Airtel serikalini.
Alisema TTCL imeendelea kujiendesha kwa faida, ambapo alitoa mfano wa robo ya mwaka huu iliyoishia Septemba, ambapo faida iliyopatikana kutokana na mfumo wa uendeshaji ilifikia Sh bilioni 1, huku faida kabla ya kodi ikiwa ni Sh bilioni 2.66, na faida bada ya kodi Sh bilioni 1.8, wakati kodi iliyolipwa ikikaribia Sh milioni 800.
Share:

Spika EALA aahirisha bunge kupisha maridhiano


SPIKA wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA), Martin Ngoga amelazimika kusitisha shughuli za Bunge hilo hadi hapo zitakapoitishwa tena baada ya wabunge wa Tanzania na Burundi kutangaza kutomtambua.
Ngoga alitangaza kusitishwa kwa shughuli za Bunge hilo jana na kusema hawezi kuruhusu likaendelea kwa hatua za kuchagua wajumbe wa kamati zake, huku nchi nne tu za Sudan Kusini, Rwanda, Kenya na Uganda zikishiriki na nchi nyingine mbili zikisusa.
"Siwezi kuendelea na bunge hili kwa sababu ya akidi kutotimia, maana hatutaweza kuchagua kamati mbalimbali kutokana na mzozo wa kutonitambua mimi kama Spika. Naahirisha Bunge hili hadi hapo mtakapotangaziwa rasmi,” alisema. Hata hivyo, wakati Spika huyo alipolazimika kuahirisha Bunge hilo, tayari wabunge walikuwa wamefanya kazi ya kuchagua Kamati ya Uongozi na ndipo baadaye Bunge likaahirishwa.
Juzi wabunge wa EALA kutoka Tanzania na Burundi, walitangaza rasmi kutomtambua na kushirikiana na Spika Ngoga kutoka Rwanda, aliyechaguliwa juzi na wabunge kutoka nchi nne, badala ya sita zinazounda Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).
Akizungumza kwa niaba ya wabunge wa Tanzania, Dk Ngwaru Maghembe alisema wabunge wa mataifa hayo manne, waliendesha uchaguzi bila kuhusisha wenzao wa nchi mbili za Tanzania na Burundi wakati wanajua wanakiuka Kanuni na Sheria za Mkataba wa EAC.
Alisema wabunge wote wa Bunge hilo walipofika Arusha, walipewa fomu za kuomba kuwania nafasi ya Uspika katika Bunge hilo na ndio maana wabunge kutoka nchi tatu, ambao ni Adam Kimbisa kutoka Tanzania, Ngoga kutoka Rwanda na Leontine Nzeyimana kutoka Burundi, walichukua fomu kuwania nafasi hiyo kwa vile Kanuni zinaruhusu.
"Sheria ya Mkataba wa EAC Kifungu cha Namba 6 (c) inafafanua kuwa watafanya uchaguzi kwa maridhiano na si kufuata silabi za nchi, bali kila mtu ana haki ya kugombea nafasi hiyo kwa kila nchi," alisema.
Mbunge Dk Abdullah Makame wa Tanzania alisema Katibu wa Bunge hilo, Kenneth Maddete amekiuka Mkataba wa EAC na Kanuni za EALA na zinazotamka kuwa kutakuwa na hoja ya kupiga kura ili kumchagua Spika. “Ndiyo maana Katibu wa Bunge la EALA, Maddete alieleza kuwa wagombea watatu walikuwa wamechukua fomu kuwania nafasi hiyo ya uspika, kwa vile anajua Kanuni na sheria zilikuwa zinawapa haki ya kupigiwa kura.
"Tunahitaji jumuiya ya utashi wa kisiasa na moyo wa kuvumiliana, ndio maana tuliwasubiri wenzetu wa Kenya tukachelewa kuanza Bunge.” Alisisitiza kuwa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, pia ipo na itatumika katika kutoa ufafanuzi juu ya jambo hilo la uchaguzi wa Spika. Mwenyekiti wa wabunge kutoka Burundi, Victor Burikukiye alisema hawamtambui Spika huyo kutoka Rwanda.
Alisema watu wanaweza kutafsiri vile wanavyojua, lakini Katibu Mkuu wa EALA alitoa barua kwa wabunge watatu kuwania nafasi hiyo kwa kujua kuwa wanayo haki. "Huu ni uchaguzi gani wa nchi nne kufanya uchaguzi na tunasema hatutambui uchaguzi wa Spika uliofanyika bila ya kuwepo kwa wabunge wa Burundi," alisema.
Spika anachaguliwa kwa mzunguko na sasa hivi uspika ulikuwa ni zamu ya Burundi, Rwanda na Sudan Kusini na hii nafasi hii ilikuwa ni yetu ya Burundi, kwanini watufanyie hivi,” alisema. Mbunge kutoka Uganda, Chris Opoke alisema wabunge hao wamepoteza miezi sita bila kuanza kwa bunge, hivyo hawaoni sababu ya kuchelewa tena kuendelea na bunge hilo kwa sababu ya kukosekana kwa spika, hivyo aliunga mkono Spika huyo kuchaguliwa.
Share:

Tanzania yawa ya kwanza kutumia taasisi za fedha


WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amewataka wananchi kujenga tabia ya kujiwekea akiba ya fedha kwenye taasisi za kifedha kwa kuwa ni nguzo muhimu kwa maendeleo yao. Aliyasema hayo jana Dar es Salaam wakati akizindua Mpango wa Pili wa Taifa Huduma Jumuishi za Fedha wa Mwaka 2018 hadi 2022.
Alisema katika Mpango wa Kwanza wa Taifa wa Huduma Jumuishi wa mwaka 2014-2016, mafanikio makubwa yamepatikana ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa asilimia 86 mwaka 2017, kutoka asilimia 29 mwaka 2012 ya wananchi walio karibu na huduma za kifedha.
Kwa mujibu wa Waziri Mkuu, idadi ya Watanzania wanaotumia huduma za kifedha nchini imefikia asilimia 65 na kuifanya Tanzania kuwa ya kwanza barani Afrika na ya sita duniani kwa kuboresha mazingira ya upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wananchi.
Ili kuhakikisha Mpango huo wa Pili wa Taifa wa Huduma Jumuishi za Fedha unafanikiwa katika kuwafanya wananchi kujenga tabia ya kujiwekea akiba ya fedha, Waziri Mkuu alisema, “Tunataka kuongeza kiwango cha wananchi wanaojiwekea akiba ya fedha kupitia mifumo rasmi kutoka asilimia 43 mwaka 2017 hadi kufikia asilimia 60 mwaka 2022.
“Kuongeza kiwango cha wananchi kuwa karibu na huduma za kifedha katika umbali usiozidi kilomita tano kutoka asilimia 86 ya mwaka 2017 hadi kufikia asilimia 90 mwaka 2022; kuongeza kiwango cha wananchi wanaotumia mara kwa mara huduma za kifedha kupitia asasi za fedha na mitandao ya simu kutoka asilimia 65 mwaka 2017 hadi kufikia asilimia 75 mwaka 2022.”
Malengo mengine ya Mpango huo wa Pili kwa mujibu wa Waziri Mkuu ni kuongeza kiwango cha wananchi wanaotumia huduma za bima kutoka asilimia 45 mwaka 2017 hadi kufikia asilimia 50 mwaka 2022, kuongeza kasi ya kuwawezesha wananchi kuwa na vitambulisho vya taifa kutoka asilimia 23 mwaka 2017 hadi kufikia asilimia 90 mwaka 2022.
Aidha, alisema kuwa kupitia mpango huo, serikali inataka kuongeza matumizi ya mifumo ya kielektroniki katika kutoa huduma za kifedha nchini. Alisema mpango huo wa Huduma za Kifedha ni muhimu kwa kuwa utalisaidia Taifa katika ujenzi wa uchumi wa viwanda, kukuza uchumi wa wananchi na kupunguza umaskini. Kutokana na umuhimu wa mpango huo, Waziri Mkuu alisema serikali inasisitiza kuendelea kuwepo kwa ushirikiano imara kati ya sekta binafsi na sekta ya umma.
Alisema serikali itaendelea kuimarisha miundombinu kama vile ya umeme, kuweka mazingira wezeshi ya huduma za kifedha ili kuondoa vikwazo kwa watoaji na watumiaji wa huduma za kifedha nchini. Kwa upande mwingine, serikali imewataka wajumbe wa Baraza la Taifa la Mpango Huduma Jumuishi za Kifedha kutoa elimu kwa umma kupitia njia mbalimbali kama vile vyombo vya habari na makongamano ili wananchi wengi wajue umuhimu wa huduma za kifedha kwenye maisha yao.
Share:

Mnada Mirerani waiingizia Serikali bilioni 2


KAMPUNI ya TanzaniteOne na Shirika la Madini la Taifa (Stamico) wamefanikiwa kuuza madini yenye thamani ya Sh bilioni 1.8 katika mnada uliofanyika kwa mara ya kwanza katika kijiji cha Naisinyai kilichopo wilayani Simanjiro mkoani Manyara.
Kampuni ya TanzaniteOne na Stamico wameweza kuuza madini hayo kwenye mnada wa madini ulioshirikisha wanunuzi wa madini kutoka kampuni mbalimbali za madini hayo za ndani na nje ya nchi.
Awali kampuni mbili za wazawa ambazo ni Tanzanite Africa Ltd na ClassicGame Ltd walijitokeza kuuza madini hayo lakini waliyaondoa kutokana na kutoridhika na bei iliyokuwa sokoni na hatimaye Kampuni za TanzaniteOne na Stamico walifanikiwa kuuza madini hayo.
Akitangaza matokeo ya mnada huo, Kamishna wa Madini nchini, Benjamin Mchwampaka alisema kuwa jumla ya gramu 47,201. 00 za tanzanite ghafi ziliuzwa kwa dola za Marekani 820,744. 00.
Alisema kutokana na mauzo hayo serikali inatarajia kukusanya mrahaba na ada ya ukaguzi dola za Marekani 57,452.08 sawa na Sh milioni 128.8. Alisema pia Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro inatarajia kulipwa Sh milioni 5.5 kwa kodi na huduma.
Naye Naibu Waziri wa Madini, Stanislaus Nyongo alisema wanampongeza Rais John Magufuli kwa kutangaza mnada huo wa madini kufanyika mkoani Manyara ili kufungua fursa za biashara katika eneo hilo.
Pia alisisitiza kuwa suala la kudhibiti utoroshwaji wa madini hususani ya tanzanite ni mojawapo ya hatua zilizochukuliwa, ikiwemo kujengwa kwa ukuta kwa kuzunguka eneo la mgodi ya tanzanite wenye urefu wa kilomita 24.5.
Alitoa rai kwa wachimbaji wa madini kuhakikisha wanashiriki katika mnada huo mara kwa mara ili waweze kuuza madini yao ya tanzanite. Awali Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Alexander Mnyeti alisema kuwa kampuni 12 zinazochimba madini ya tanzanite eneo la Mirerani zinadaiwa kiasi cha Sh bilioni 3 baada ya kudiriki kukwepa kulipa kodi serikalini.
Alisisitiza kuwa serikali haitasita kuwachukuliwa hatua za kisheria wachimbaji wengine wa madini hayo ya tanzanite kwani ni lazima walipe kodi ili waweze kufanya biashara zao. Naye mmoja wa Wakurugenzi wa Kampuni ya TanzaniteOne, Hussein Gonga aliipongeza serikali kwa kuwezesha mnada huo kufanyika kwa mara ya kwanza kwenye eneo hilo na kufungua fursa ya biashara kwa wakazi wa eneo hilo.
Share:

Popular Posts

Followers

Search This Blog

My Blog List

Labels

Contributors

Recent Posts

Pages